Monday, December 23, 2013

KILIO CHA MWENYE HAKI!!!



Leo nataka niseme juu ya KILIO. Kuna tofauti ya kulia kwa machozi ya nje na kulia kwa machozi ya ndani. Mtu anapotendewa kitu na ndani yake akasikia KUNYANYASIKA na akasikia uchungu sana, mara nyingi anatoa machozi ya nje (atalia). Lakini sio kila mara mtu atalia kwa machozi, ila kuna ule UCHUNGU wa ndani ambao watu mbalimbali wamekua nao na wameenda mbele za Mungu kwa maombi au hata wametamka tu maneno na Mungu AMESIKIA (“nipo pamoja nanyi katika mipango yenu, kabla ya kuomba mimi Bwana nitasikia na mkiwa katika kunena mimi Bwana nitajibu”). Chunga hii kitu, Mungu anasikia KILIO kuliko unavyodhani. Na mara nyingi sana hiki KILIO hata kama mtu sio mlokole nakwambia UKIMDHULUMU, UKIMNYANYASA, UKIMTENDA JEURI mtu na akalia kwa UCHUNGU mbele za Mungu hata kama hakumwambia mtu au hata kama hajui kama Mungu anasika, nakwambia Mungu husikia VILIO.

Wakati Mungu anamtokea Musa na anamtuma Misri kuwakomboa wana wa Israel kutoka UTUMWANI, Mungu alisema “nimesikia kilio chao nami nimeshuka kuwakomboa”. Mungu hakusikia maombi bali KILIO! Sasa ninataka uone huu mfumo vizuri. Pale Misri wana wa Israel walikua watumwa, na juu yao kulikua na VIONGOZI na WASIMAMIZI na kule juu kabisa alikuwepo Mfalme Farao. Kiutawala hawa watumwa walikua chini kabisa, ila walikua WANA wa MUNGU aliye hai. Kumbuka “hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu na ile iliyopo imeamriwa na Mungu”. Kwa lugha ya kawaida BOSS mkubwa sana katika “utawala wowote” hapa duniani ni Mungu. Sasa kama mtu mwenye HAKI, amefika mahali pa gumu sana na amelia kwa MATESO mbalimbali, akiwa hajui huu mfumo bado BOSS mkubwa hushuka hapo na kurekebisha mambo, haleluya! Kwa wale wanajua hii SIRI na kusimama katika nafasi na zamu zao vizuri, HAWATAMSUJUDU boss wao wa duniani na kufanya NGONO, nk., na kumkosea Mungu kwa sababu ya kulinda MASLAHI yao ya kikazi. Watapambana kwa “NIA ya kushinda UOVU na KUTII kwao kutakapotimia MAMLAKA yao katika ulimwengu wa roho dhidi ya wakuu wa giza na majeshi ya pepo wa baya ITAONGEZEKA sana”. Na KILIO chao Mungu atasikia na ATASHUKA kuwaokoa. Kumbuka, Mungu ndio boss mkubwa pale juu ila maandiko yanatuonya TUTII mamlaka iliyo kuu. Na usithubutu kumwambia kiongozi wako kuwa wewe sio boss ila boss ni Mungu. Jua hilo moyoni na mtizame Mungu kama Mkuu wako wa kazi na chapa kazi kwa moyo, acha uvivu.

Nebkadneza mfalme wa Babeli alikwenda kula majani miaka/misimu 7 kwa kosa la kujisifia kwamba “huu mji ni mkono wangu umejenga?” Akatizama mafanikio ya Ufalme (kampuni yake) akajiinua ndani ya moyo wake! Mungu akasema sasa utajua kwamba mimi natawala pamoja na wanadamu, sio wewe Nebkadneza, ni Mimi! Hii siri watu “wachache” wanaijua na wamehusika kuwapiga “transfer” (uhamisho) mabosi wao kwa sabababu wameleta shida kwenye KAMPUNI na jina la Mungu linatukanwa au watu wamenyanyaswa. Transfer inaweza kuwa kulala, kushushwa cheo (kula majani), kuhama kituo cha kazi, nk. Ila vita vyetu sio juu ya DAMU na NYAMA. Ni katika roho, na tunapata NGUVU tukiwa na NIA thabiti ya kupinga UOVU wote na KUTII kwetu kutakapotimilika (2Kor. 10:4-6). CHUNGA sana usije ukafanya mambo kwa HUSUDA, WIVU au MASHINDANO, utashindwa. Mamlaka ya Mungu haifanyi kazi hapo. LAZIMA usimame katika KWELI na HAKI na sio maslahi binafsi. Usikubali kumkosea Mungu kwa kisingizio eti “sasa huyu ni MHESHIMIWA na mimi ningefanya je?”, mwite Yesu hapo akuokoe na KILA (hata kama sio mlokole) atakayeliitia jina la BWANA ataokoka katika hali anayopitia. NEEMA ya BWANA izidi KWENU. AMEN

Frank Philip.

No comments:

Post a Comment