Sunday, December 8, 2013

NJIA YA WOKOVU!!!


Kwenye maaandiko tunajifunza kwamba watu walioanza kumfuata Yesu wakati huo wa Mitume hawakuitwa Wakristo bali waliitwa “watu wa NJIA”. Kati ya namna mbalimbali ambazo Yesu kujitambulisha, mojawapo alijiita yeye ni NJIA. Na akasema hii NJIA inatufikisha wapi. “mimi ndimi njia ya Kweli na Uzima, mtu haji kwa Baba ila kwa kupita kwangu”. Hakuna njia isiyomfikisha mtu mahali fulani. Kila mtu anachagua njia kwa makusudi ya kufika mahali fulani, awe anapenda au hapendi ila kitakachomfanya afike hapo MAHALI ni njia aliyojichagulia. Yesu anashauri na kutualika akisema “ingieni kwa kupitia mlango ulio mwembamba; maana mlango ni mpana, na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache.” (Mathayo 7:13, 14)

Nataka tujifunze hii njia ya Yesu. Hii njia ina sifa nyingi zisizovutia isipokuwa sifa moja kwamba itakufikisha kwa Baba. Kwanza watu watakaoiona hii njia ni wachache achilia mbali watakao pita juu yake. Sasa kusudi la njia ni kupita/kutembea na wala sio kukaa au kusimama. Unapoitwa kwa Yesu, ukakubali na “kukata shauri” KUMFUATA, jua umepata MWALIKO wa kutembea katika hii NJIA. Kupata mwaliko haina tofauti na kupata TIKETI ya kusafiria. Usipochukua hatua na kupanda basi huwezi kuona mambo yaliyoko njiani. Utajifariji na tiketi yako mkononi kwa sababu imeandikwa UNAKOKWENDA ila usipoanza safari hufiki huko japo pameandikwa kwenye tiketi yako.

Sifa moja ya muhimu sana ya NJIA “hii” ni wembamba wake. Tunaambiwa IMESONGA. Kuna tofauti ya wembamba na kusonga. Katika mawazo yangu napata picha ya njia ambayo iko katikati ya kuta ndefu kila upande. Kwa lugha ya kawaida ningeiita “uchochoro”. Yaani ni nyembamba lakini pia imesongwa na kuta huku na huku. Ukiwa na MAFURUSHI makubwa UNANASA hapo kwa sababu kumesonga sana. Hii hali ya kusonga/kubana huwezi kuiona kama HUJAANZA safari. Ukisikia mtu anasema WOKOVU ni “tambarare” jiulize kwamba anapita njia gani? Maana huku kumebana, yeye tambarare anaipata wapi? Bwana wetu mwenyewe alisema “ulimwenguni mnayo dhiki lakini jipeni moyo, mimi nimeushinda ulimwengu”, sasa alishinda nini kama kila mahali ni tambarare na hakuna vita?

Sasa kuna mambo mengi sana ukiyaangalia utagundua yanakupasa kufanya KAMA umeanza safari ya kumfuata YESU. Kwanza NJIA inaelekeza uelekeo (direction) ambao hujachagua wewe ila mwenye njia (Yesu). Utagundua kwamba huwezi kubeba kila kitu (kiburi, tamaa mbaya, uzinzi, uchungu, kutokusamehe, etc.) ukafanikiwa kupita kwa sababu njia imesonga. Kwa sababu hii njia ni ya kufikirika (theoretical/hypothetical) japo ni dhahiri (practical/real) wakati wa kupita inakuwa ngumu kuonekana na wachache wataiona pale watakapochukua HATUA. Usipochukua hatua na kuanza safari huwezi kuelewa maana ya KUSONGA!

Kuna mambo manne MUHIMU yatakatokuwezesha kutembea katika NJIA hii. La kwanza, kumpokea Yesu kama Bwana na Mwokozi wa maisha yako, kutubu na kugeuka. La pili, kujazwa Roho Mtakatifu. Roho Mtakatifu sio NGUVU ila ni NAFSI ya Mungu japo pia Ana NGUVU. Roho Atakufundisha yote, kukukumbusha pia kukufariji uwapo njiani (hutakua yatima ujapopita nyikani). La tatu, kusoma Neno kwa BIDII tena KILA siku. Kama unavyokula chakula cha mwilini, lisha na roho yako ipate nguvu. Neno lina nguvu ya kukutakasa na kutenda mapenzi ya Mungu maishani mwako. La nne, DUMU katika maombi ili usianguke MAJARIBUNI na upate mwongozo (direction) uwapo safarini. Huwezi kutenda mapenzi ya Mungu kama wewe sio muombaji.


Kama hujasikia KUBANWA/KUZONGWA anza kujiuliza swali hili, Je! Umeanza safari? Na kama umeanza, jiulize tena Je! Hujabanwa/hujanasa kwa sababu umetua kila mizigo ya dhambi, uchungu, nk.? Kama unajua bado kuna shida ndani yako na hujatengeneza vizuri mambo na “kutaka amani na watu wote na huo utakatifu”, jiulize tena swali, Je! Uko njia nyembamba au pana? Ukipata majibu ya hayo maswali chukua hatua zipasazo.

Mambo muhimu ya kukumbuka ukiwa NJIANI (safarini). Kuna vibao vingi sana vya kukupoteza (DIVERSIONS). Kuna kona nyingi (mambo magumu na mateso) na njia-panda nyingi (mahali pa kuchagua kumtii Mungu au Ibilisi) na mara nyingi njia-panda (makutano ya barabara) hayako kwenye mteremko, ila yako kwenye mwinuko. Baada ya kuchoshwa na “safari”, unafika njia-panda, kushoto (kwa Ibilisi) ni mteremko na kulia (kwa Yesu) ni mlima zaidi! Kama UMEKAZA uso wako kwa Yesu, utapita KONA zote, na ukifika NJIA-PANDA utapinda kuelekea tena kwenye NJIA nyembamba (kwa Yesu) hata kama huko mbele ni MLIMA zaidi.

Ukizidi kuendelea na safari utagundua kuna MABANGO makubwa yameandikwa jina lako. Mengi ya haya mabango yamebeba lugha ya kukebehi, matusi, kukatisha tamaa, kukera, nk. Usiangalie MABANGO, kaza uso wako kwa Yesu kama Stefano. Sio rahisi, hata Yesu amesema sio rahisi ila njia inapitika. Wakati Stefano anapigwa mawe, hakukimbia badala yake alipiga magoti. Akatazama juu USHINDI wake ulipo! Hakutizama warusha mawe (MABANGO), hakusikiliza wanayosema wakati wanarusha mawe (ujumbe kwenye mabango), aliangalia JUU. Badala ya kuwarushia maneno ya LAANA, Stefano alikua busy kuwaombe watesi/wauaji wake msamaha. Wakati watu wanaona damu inatiririka mwilini mwake, Stefano alimwona Yesu na Jeshi la malaika watakatifu. Wakati watu wanaona mauti, Stefano anaona UZIMA wa MILELE! Akakaza USO wake kwa BWANA na kumaliza SAFARI yake salama.

Jiulize ni watumishi wangapi leo wataambiwa wana BELIZEBULI wasipigane ngumi? Jiulize ni wana wa Mungu wangapi leo wakinenewa tu jambo hata kama ni la uongo wanakwazika na kuwa wakali? Eti wanachafuliwa majina na kuvunjiwa heshima! Sawa, ila mtizame yeye aliyejiita “NJIA” ambaye tunamfuata,“Yesu, hali akijua ya kuwa Baba amempa vyote mikononi mwake, na ya kuwa alitoka kwa Mungu naye anakwenda kwa Mungu, aliondoka chakulani; akaweka kando mavazi yake, akatwaa kitambaa, akajifunga kiunoni. Kisha akatia maji katika bakuli, akaanza kuwatawadha wanafunzi miguu, na kuifuta kwa kile kitambaa alichojifunga.” (Yohana 13:2-4). Yesu alipogundua ana KILA KITU (kwa lugha ya kawaida tungesema UTAJIRI wa kila namna), na yuko kwenye njia (safarini) “Yesu, hali akijua ya kuwa Baba amempa vyote mikononi mwake, na ya kuwa ALITOKA KWA MUNGU NAYE ANAKWENDA kwa Mungu” akijua hayo, alivua VAZI lake (sio kukunja shati mikono au kukunja suruali), akajifunga kitambaa kiunoni, akachukua maji (hakumtuma mtu akalete kwa maana wakati huo alikuwa ni MTUMISHI anayetumika), akainama, akawanawisha na kuwafuta kwa kitambaa (nguo iliyo mwilini mwake)! Huyu ni Bwana na NJIA tunayoifuata.

Ujumbe huu umekuja kukumbusha habari ya NJIA na yatupasayo kufanya katika NJIA hii. Mungu atupe NEEMA ya kujikagua na kupata UTHIBITISHO wa ndani kwamba tuko njiani au la! Roho anashuhudia pamoja na roho zetu kama sisi ni wana wa Mungu, naye Atatupa kutambua kwamba tuko katika njia gani kwa maana haachi kushuhudia juu ya “DHAMBI, HAKI na HUKUMU”. Msikilize Roho Mtakatifu na MAELEKEZO yote atakayokupa, UTAFIKA salama kwa BABA.

NEEMA ya BWANA wetu YESU KRISTO iwe nanyi tangu sasa na hata MILELE AMEN.

Frank Philip.

Saturday, December 7, 2013

MWALIKO WA KUHUDUMU!!!


Watumishi wa Mungu wengi sana hawaendi mahali kufanya HUDUMA hadi wapewe mwaliko rasmi na kutimiziwa baadhi ya masharti ikiwemo KISI fulani cha malipo au gharama. Sipingi kulipiwa gharama kwa sababu maandiko yanasema “watahubirije kama hawakupelekwa?”

Ninachotaka kuweka wazi hapa ni aina tatu za MIALIKO. Mwaliko wa kwanza, kuna wakati hujaalikwa na mtu kwenye huduma/kanisa lake ila Mungu amekualika kwenda kufanya kazi maalumu. Mwaliko wa pili, kuna wakati hujaalikwa na Mungu ila watu wanataka ukahudumu kanisani/mahali fulani. Na mwaliko wa tatu, kuna wakati utakua umealikwa na Mungu kufanya huduma na watumishi wa mahali hapo hawajakualika. Aina zote hizi za mialiko huwezi kukwepa kama wewe ni mtumishi wa Mungu, au Mwana wa Mungu kwa sababu WOTE tumeitiwa KUSUDI maalimu katika mwili wa Kristo, uwe unajua au hujui.

Umewahi kujiuliza ni mara ngapi Yesu amealikwa hekaluni kuhubiri? Kwanza wale wakuu wa DINI walikua wanatafuta namna ya kumfungia mahali hata asitembee licha ya kuhubiri hekaluni kwao. Lakini Baba yake “alimwalika” kufanya huduma na alienda MAHALI alipotakiwa na KUTIMIZA kusudi bila kusubiri “watu” kumwalika. Angalia mitume 11 wa Yesu, walikua wanawindwa na kuonekana ni VICHAA na wenye PEPO. Watu waliochanganyikiwa na wasifaa katika jamii. Wakuu waliwaona kwama mahali pa kuwafaa ni jela! Lakini ilikua ikifika “saa ya sala” utawaona wako hekaluni. Sasa usifikiri walikua wanapewa tu nafasi kule mbele kwenye viti maalumu na kuhehimiwa! No! walikua wanafanya kazi ya Mungu katika mazingira yoyote “wakati ufaao na wakati usiofaa”.

Sitaki nikupe ushuhuda binafsi lakini kwa sehemu tu nataka nikwambie mimi binafsi nimeenda mahali pengi sana bila kualikwa. Mara nyingine sikusema hata neno moja na mara nyingi hata “wenyeji” hawakujua kama nimwo katikati yao, ila huwa nahakikisha nimeacha MBEGU na FOOT PRINTS kwamba kuna “mtu wa Mungu alipita hapa”. Kuna idadi kubwa sana ya Watumishi wa Mungu wako namna hii na nimeona niweke hii SIRI hadharani ili usikae tu pale KANISANI au MAHALI popote kama boga. Wala usishawishi watu WAKUALIKE na kukupa nafasi za Mbele, Muulize Mungu kusudi lake na nini anataka ufanye kwa wakati huo. Matokeo ni mkubwa sana sana katika ulimwengu waroho ukitembea namna hii.

Ukiona mtu anafugwa kwenda mahali eti kwa sababu hela haijaingia kwenye accounti yake ya benki, jiulize swali hili, Je! Hana nauli? Na kama nauli anayo na amegoma kwenda kwa sabau hela haijaingia kwa account yake, juilize tena swali, Je! Anamtumikia nani? Kama anamtumikia Mungu, tena jiulize swali, Je! Amealikwa na Mungu au wanadamu? Na kama amealikwa na Mungu, jiulize tena swali, Je! Anatenda MAPENZI ya nani? Haya majibu ni kwa matumizi binafsi na ujipange sawasawa kuyajibu kama wewe unatarajia UZIMA wa MILELE.

Namaliazia kusema kwamba, MIALIKO maalumu ni michache sana. Mavuno yako tayari na ni MENGI. Bwana wa mavuno anasema “watenda kazi ni wachache”. Kwa bahati mbaya, hawa watendakazi wachache pia wanasubiri mialiko maalumu! Funguka Macho ya Rohoni kwa Jina la Yesu.

Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na Ufunuo wa KWELI ya Mungu uwe nasi sasa na hata MILELE. AMEN.

Frank Philip.

Friday, December 6, 2013

JIFUNZE JINSI YA KUMUONA MUNGU AKIJIDHIHIRISHA KWAKO!!!


Mara nyingi sana tumeona watu wanatamani kumwona Mungu akijidhihirisha katika maisha yao, hata ikiwezekana kwa ngurumo na matetemeko, ila kila mahali ni kimya kama Mungu hayupo. Nataka nikupe SIRI moja kati ya nyingi ambazo zinaweza kukusaidia.

Umewahi kujiuliza nini kinatokea wakati Mungu anatafuta watu wa kujidhihirisha kuwa mwenye NGUVU hawaoni! na upande mwingine watu wanatafuta UDHIIRISHO wa Mungu kwenye maisha/huduma zao hawaoni kitu pia? Tunafahamu kwamba “Kwa maana macho ya Bwana hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake. Kwa hayo umetenda upumbavu; kwani tangu sasa utakuwa na vita.” (Mambo ya Nyakati 16: 9)

Kwa upande mwingine kila mtu anajua na kukiri kwamba Mungu yuko karibu sana kuliko hata pumzi yake, nk. lakini kwa kweli anasema tu huku hata akiomba inakuwa kama Mungu yuko ng’ambo ya bahari au Mbingu imepauliwa kwa zege. Hata inafika watu wa Mungu wanaamua “kuteremkia Misri” (kufuata njia za kidunia kama rushwa, nk.) ili kupata msaada, kwanini? Wanaona Mungu yuko mbali na wanaona kila kitu mbele yao ni milima na bahari tu na hawawezi kuvuka hapo. Ghafla! Wanaanza kujirahisisha na kufanya dhambi kama vile Mungu hayupo. Huku tunaambiwa Mungu ni SHAHIDI mwepesi! Sasa mbona inakua NGUMU kujidhihirisha na matendo yake MAKUU akitutetea kama ni shahidi MWEPESI? “Nami nitawakaribieni ili kuhukumu; nami nitakuwa shahidi mwepesi juu ya wachawi, na juu ya wazinzi, na juu yao waapao kwa uongo; na juu yao wamwoneao mwenye kuajiriwa, kwa ajili ya mshahara wake, wamwoneao mjane na yatima, na kumpotosha mgeni asipate haki yake, wala hawaniogopi mimi, asema Bwana wa majeshi.” (Malaki 3: 5)

Sikiliza kwa makini, Mungu sio mwanadamu, Yeye anaona “NIA iliyoko ndani yetu”. Weka moyo wako vizuri juu ya mambo uombayo ama sivyo hupati kitu. “Mwatamani, wala hamna kitu, mwaua na kuona wivu, wala hamwezi kupata. Mwafanya vita na kupigana, wala hamna kitu kwa kuwa hamwombi! Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu. Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.” (Yakobo 4:1-3)

Sasa utakuta wana wa Mungu wamefika mahali wamejichanganya sana. Nusu kwa Mungu nusu mtaani/kwa Ibilisi. Halafu unatarajia udhihirisho wa Mungu kwa radi na matetemeko. Utakuta mtu anakiri ushindi pale tu anapotaka KITU kwa Mungu ila akijaribiwa KUTENDA dhambi anakua mpole wala hafungui kinywa! Hadi anazini, kula rushwa, kusema uongo, nk. halafu baadae anatubu! Ule “UKAMILIFU wa UELEKEVU wa Moyo” (Nyakti 16:9) kama wa Ayubu wakati wa majaribu uko wapi? Kama moyo wako ni MWELEKEVU kwa UKAMILIFU (soma hapo juu kifungu cha pili), wakati macho ya Bwana yanakimbia-kimbia duniani KUSAKA watu wa kujidhihirisha mwenye NGUVU, lazima yataku NASA tu na Mungu anaanza kuwa shahidi mwepesi kwako ghafla! Ila kama bado nusu moyo umeweka kwa boyfriend/girlfriend na mnafanya uchafu au ku-chart dirty stories, au upande mmoja rushwa, dhuluma, na upande mwingine Mungu, hapo sahau kuona UDHIHIRISHO wa Mungu. Utaomba na mbigu itakuwa kama chuma juu yako, utasikia kama mkiwa jangwani kwa maana Roho Mtakatifu ni Mtakatifu kweli, usitarajie umburute kama silaha tu ya kushambulia wakati UNASHIDA halafu unaishi maisha ya KUMHUZUNISHA na KUMZIMISHA. Mungu ATAWAONA na atajionyesha mwenye NGUVU sio kwa kila mtu ila “waliokamilika moyo kuelekea kwake”, na jicho lake liko busy kutafuta, kwa kukimbia-kimbia duniani kote kumsaka huyu mtu. Kwanini Mungu anafanya msako? Kwasababu hawa watu ni ADIMU!

Watu wengi wamekuwa ADUI wa Mungu bila kujijua huku wanamwita Baba! Haiwezekani unafanya urafiki na DUNIA na mambo yake halafu unatarajia Mungu ni baba yako! Ndio maana “Yesu akawaambia, Kama Mungu angekuwa baba yenu, mngenipenda mimi; kwa maana nalitoka kwa Mungu, nami nimekuja; wala sikuja kwa nafsi yangu, bali yeye ndiye aliyenituma. Mbona hamyafahamu hayo niyasemayo? Ni kwa sababu ninyi hamwezi kulisikia neno langu. Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo.” (Yohana 8:41-43).

Sasa chunga njia zako vizuri. Sisemi kila mdhaifu katika dhambi ni mtoto wa Ibilisi, tunajua kuna habari ya “Mwana lakini ni mpotevu”. Ameenda huko duniani kuishi kwa maisha ya anasa ya UZINZI lakini ni “mwana”. Tunajua habari ya Yesu kwamba kuna “kondoo” mmoja mahali nje ya zizi, amepotea, na Yesu yuko tayari kuacha hawa 99 ili AKAMSAKE huyu mmoja! Sasa nakupa shauri, kimbilia kwa Yesu haraka, kama wewe ni kondoo na unajua uko nje ya zizi au kama ni mwana mpotevu uko huko duniani, rudi kwa Baba. Weka moyo wako vizuri KUMWELEKEA yeye peke yake kwa UTIMILIFU utaona MACHO ya Mungu yakikutembelea kwa maana yanakutafuta siku nyingi na hayakuoni, na utashuhudia NGUVU zake maishani mwako kwa maana HAKIKA atajidhihirisha kwako.

Neema na Baraka zitokazo juu ziwajaze mnapozidi kuyatafakari na kuyatenda mapenzi ya Mungu. AMEN.

Frank Philip.

Thursday, December 5, 2013

MUNGU ANAONA NINI NDANI YETU?


“Mkinipenda mtazishika amri zangu” na “azipokeaye amri zangu na kuzishika, yeye ndiye anipendaye. Naye anipendaye mimi atapendwa na Baba yangu, nami nitampenda na kujidhihirisha kwake.” (Yohana 14:14,22).

“Wanafunzi wake wakaulizana, "Je, kuna mtu aliyemletea chakula? Yesu akawaambia, Chakula changu ni kufanya anachotaka yule aliyenituma na kuitimiza kazi yake.” (Yohana 4:33,34).

Nimejiuliza sana maswali kwamba Mungu huwa anatuonaje tunapokwenda mbele zake? Je! Tunajiona angalau kwa sehemu na kujitambua kwamba tukoje mbele zake?

Umewahi kujiuliza ile nguvu tunayoweka katika MAOMBI na KUFUNGA na jitihada ya kutafuta MSAADA wa maombi kwa watumishi mbalimbali wa Mungu wakati tukiwa na mahitaji ya mambo ya MWILINI kama kufaulu mitihani tukiwa shule, kupata kazi, kupanda cheo, kupata wachumba, biashara zetu kufanikiwa, kupona magonjwa, nk.? Umewahi kujiuliza ni NGUVU KIASI GANI unaweka katika MAOMBI ili uweze: kujua WITO wako, kumpendeza Mungu, kukaa katika mapenzi yake, kuishi maisha ya utauwa, nk.? Ukiweka katika mizani uzito wa MAOMBI na NGUVU tunazotumia katika mambo ya mwilini na ya Mungu unaona TOFAUTI gani?

Je! Unafahamu pamoja na Wana wa Israel kutoka Misri na kuvuka Baharini kwa ushindi, kwamba walipomkasirisha Mungu kwa matendo yao bado walifia jangwani? [kwa nyoka za moto, kumezwa na ardhi, nk.?] Je! Tunajitahidi kwenye maombi kupata mafanikio na tukiisha kuvuka kile kipindi cha shida tumdhihaki na kumtukana Mungu aliyetuvusha kwa matendo yetu maovu? Tena tunamtenda dhambi kwa kuvitumia vile vitu alivyotubariki navyo? Umewahi kujiuliza kwamba ni kwanini Mungu asikuache katika hali NGUMU ili uzidi kumtafuta maana akikuinua tu kidogo unamsahau? Mungu ni wa REHEMA na si mwepesi wa hasira, anatupa kila siku ingine tena nafasi ya kutafakari njia zetu na kuona “kama iko njia ya kuleta majuto” ndani yetu ili tumrudie KUTUBU na kumwishia.

Haya maswali yalinipeleka kuwaza JE! TUNAMWOMBA MUNGU KAMA TUNAMPENDA AU “TUNAMTUMIA” TU KWENYE SHIDA ZETU KISHA KUMWACHA? Mungu anaona tunampenda YEYE au DUNIA zaidi?

“Bali utamkumbuka Bwana, Mungu wako, maana ndiye akupaye nguvu za kupata utajiri; ili alifanye imara agano lake alilowapa baba zako, kama hivi leo.”(Torati 8:18)

NEEMA NA BARAKA ZITOKAZO KWA MUNGU BABA ZIWE NANYI TANGU SASA NA HATA MILELE. AMEN.

Frank Philip.

Wednesday, December 4, 2013

......MAANGALIZO!!!



(HATUA za HUDUMA na VIPAWA vyako)

1. Jua kutofautisha kati ya HUDUMA na BIASHARA. Msukumo wa HUDUMA hauko katika kufanya FAIDA bali kutenda kile mtu anachokifanya kwa “jamii” fulani, na hiki “kitu/shughuli” kimejikita katika Mapenzi ya Mungu. Malengo na Madhumuni ya huduma ni KUTUMIKIA sio KUTUMIKIWA. Kumbuka katika UFALME wa Mungu, hakuna aliyeacha ndugu, wazazi, au shughuli yake NYINGINE na akachagua kufanya HUDUMA katika Ufalme huu asirudishiwe mara 100! Mtihani upo katika kukaa kwa UAMINIFU na kwa SABURI ukimtizama yeye ALIYEKUTUMA na wala sio FAIDA. Ili UINULIWE unahitaji kufaulu mtihani wa UNYENYEKVU na ITAKUPASA kunyeyekea CHINI ya mkono wa Mungu ulio hodari UKISUBIRI akukweze kwa WAKATI WAKE. Huu wakati unakuja, ila ni wa kusubiri. Usidanganywe na MTU yeyote, huu ni wakati wa MAUMIVU na KUPIMWA imani yako kama kweli UKO KAZINI au unatafuta hela! UKIFAULU hapo, hakuna mahali hutakanyaga wala pesa hutapata. Hakuna ALAYE ataweza kumaliza “mavuno yako” japo kwa kweli walaji watakuwepo! Ili uweze kusimama mahali “hapa” (pa kupimwa na kusubiri kuinuliwa), katika njia ya kufikia “MAHALI pa USHINDI” wako utahitajika kufanya MAOMBI ya dhati kabisa huku ukichunga KINYWA chako maana anayekupima UVUMILIVU na IMANI yako mara nyingi sana ni YULE BWANA “unayemtumikia” ili ajue ATAKUPANDISHA cheo hadi wapi. Jinsi utakavyoshinda huu MTIHANI (interview) ndio UTAPANDA mbali zaidi.

Kumbuka mfano wa talanta (5, 2, 1), kiwango cha KUPOKEA hakikua kwa Bwana atoaye bali UWEZO wa mtumishi APOKEAYE. Ukitaka kupokea VINGI jiandae kujifua vizuri katika MAOMBI na SABURI. Huku ukila Neno kwa WINGI maana hivyo ndivyo vitendea kazi shambani mwa Bwana lakini pia ndio CHANZO cha IMANI katika Kristo. Nyenzo na vitendea kazi vya muhimu katika HUDUMA ni IMANI na MAMLAKA! Kumbuka Mamlaka inapatikana katika KUMTII Mungu katika mambo YOTE. Hivi viwili vinafanyaje kazi? IMANI ni kama FEDHA, NGUVU au UFUNGUO. Ili uweze kumiliki MAMBO fulani katika ulimwengu huu, na wa roho unahitaji hiki kitu ambacho kinaitwa IMANI. Kuna wakati utahitaji KUTEKA kambi ya adui ili ujitwalie MATEKA, bila NGUVU (imani na mamlaka) huwezi maana adui ameitwa ni “mwenye nguvu”. Kuna wakati unahitaji FUNGUO za kufunga au kufungua vitu katika ulimwengu huu na wa roho ili HUDUMA isonge mbele bila mamlaka huwezi kufurukuta.

HUDUMA inasema hivi “nimetenda ‘Mapenzi ya Mungu’ kiasi hiki na KUMRUDISHIA Mungu utukufu wake, na Mungu anasema “moja mia, au moja sitini au moja thelathini”, kulingana ni KIWANGO chako cha KUPOKEA kama MTUMISHI MWEMA na MWAMINIFU” Kwenye HUDUMA mara nyingine hakuna ulinganifu wa ULICHOPANDA na UTAKACHOVUNA kwa jinsi ya mwili. Huwezi Kupima mafanikio ya HUDUMA kwa kiwango cha PESA japo ukifanya HUDUMA LAZIMA pesa ije. Kipimo ni KIASI cha kutenda MAPENZI YA MUNGU. Ndipo huyu atapanda MBEGU ile ile katika UDONGO ule ule, huyu atavuna 100, mwingine 60 na mwingine 30!

Msukumo wa BIASHARA ni kupata PESA. Biashara inasema “nimewekeza kiwango ‘hiki’ na FAIDA lazima iwe ‘hivi’ la sivyo ni HASARA”. Sasa kumbuka kuna WATUMISHI wengi sana wanafanya KAZI ya MUNGU kama BIASHARA. Kipimo cha Mafanikio yao ni IDADI ya BIDHAA walizozalisha na kiwango cha PESA iliyoingia. FURAHA yao sio KUFANYA mapenzi ya Mungu ila ni faida wanayopata katika KAZI ya mikono yao. Mara nyingi sana WATUMISHI wa namna hii huchanganya BARAKA za MUNGU na MALI! Yaani mwenye ‘NAZO’ zaidi AMEBARIKIWA zaidi kuliko mwenye VICHACHE! Ndio maana BWANA wangu aliita kuna WACHUNGAJI wa MSHAHARA na wachungaji wa KWELI (Mchungaji mwema). Mtumishi ambaye anafanya biashara, kitu cha kwanza sio “KONDOO” (mapenzi ya Mungu) ila MSHAHARA (pesa). Sasa hiki ni KIPIMO kigumu sana na kimefichwa mbali na huwezi kuona kwa macho ya nje, ILA Mungu aonaye SIRINI hujua ni nani anafanya HUDUMA na ni yupi anafanya BIASHARA. Sasa kumbuka, haya makundi mawili yote yataleta MATUNDA kwa Ufalme wa Mungu, tofauti yao ni kitu kinaitwa THAWABU! Thawabu hulipwa MBINGUNI na MSHAHARA hulipwa DUNIANI. Hili kundi la WAFANYA BIASHARA watapata MSHAHARA (PESA) wao na Yesu akasema “wameshalipwa duniani”. Tabia yao ni kusimama MAHEKALUNI, KUPAZA SAUTI, KUSIMAMA kwenye KONA za NJIA na kuvaa KANZU NDEFU ili watu wawaone na sio MUNGU awaone”. KUJIONYESHA na MASHINDANO ya mwilini ndio JADI yao. Sawa, watashinda na kupata PESA, ila thawabu yao huko Mbinguni ni sifuri maana wamekwisha kupokea kwa WANADAMU sifa na utukufu! Wale wanaofanya HUDUMA mara ZOTE ni wanyenyekevu wa moyo, wanatanguliza Mapenzi ya Mungu na wanaogopa KUJISIFU na kugusa UTUKUFU wa Mungu. Maombi na kufunga ni sehemu ya MAZOEZI yao RASMI ya huduma, tena CONSTANTLY na sio wakati wa MATAMASHA tu. Kumbuka HUDUMA ni MAISHA sio EVENT! Hili kundi la wafanya HUDUMA mara nyingine hudhulumiwa na kulipwa kidogo (nusu pesa kama yule mama aliyeweka sarafu kwenye sanduku la hazina na Yesu akasema, “hiyo ni zaidi kuliko zile matajiri walizotoa”) lakini FAIDA yao ni KUBWA kama wametenda mapenzi ya Mungu na kurudisha UTUKUFU wake bila kuugusa hata tone. Hili kundi ni la muhimu sana kwa maana linazaa double double. MATUNDA hapa duniani na Uzima wa milele. Ila kundi la WAFANYA BIASHARA linazaa matunda hapa duniani na kukosa UZIMA wa milele! Kwa maana hata kwa MZAHA Yesu atahubiriwa na miujiza itafanyika ila wale watendao hayo watapotea milele! Chagua kukaa katika MSTARI wa Mungu usifanye kazi ya HASARA Mtumishi wa Mungu. Kila mtu na ajipime kazi yake mwenyewe na AJITAMBUE na kujipanga sawasawa asije akasema HAKUJUA! Maana usishangae Yesu anakutembelea na KIKOTO halafu usiamini, maana wale watu waliofanya biashara hekaluni wakati “ule” hawakumjua Yesu kama “mchapaji” pia! Chunga sana, Yesu ni yeye yule JANA, LEO na hata MILELE.
Matendo ya Mitume 20: 33 “Sikutamani fedha wala dhahabu, wala mavazi ya mtu. 34 Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami. 35 Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea. 36 Alipokwisha kunena haya akapiga magoti, akaomba pamoja nao wote. 37 Wakalia sana wote, wakamwangukia Paulo shingoni, wakambusu-busu, 38 wakihuzunika zaidi kwa sababu ya neno lile alilosema, ya kwamba hawatamwona uso tena. Wakamsindikiza hata merikebuni.”

Kuna vipawa vingine vitatumika sio kama HUDUMA bali BIASHARA. Sasa, kama Mungu amekupa kufanya biashara au kazi ya kukuingizia KIPATO kwa namna yoyote USIMSAHAU Mungu katika biashara hiyo. Tafuta makusudi yake na hakikisha BISAHARA yako INAMTUKUZA Mungu na inaheshimu na KUTII makusudi ya Mungu. Kama Mtumishi wa Mungu katika BIASHARA yako, jifunze kutafuta kusudi la Mungu na kukaa chini ya uongozi wa Roho Mtakatifu daima. Chunga sana unavyowahudumia watu na kuweka viwango vya BEI na tozo mbalimbali. “Mungu hapendi mizani za uongo”. Pima kazi na malipo kwa ulinganifu na “usichukue zaidi ya ikupasavyo”. Na jua kwamba sio kila mara utafanya kazi/biashara kwa MASLAHI ya kibinadamu (kazi au bidhaa kuuzika kwa bei ya faida kwa namna ya kibiashara). Ukijikuta unasukumwa kufanya kitu CHOCHOTE kwa pesa tu, jua unakaribia mahali pa gumu. Ukisikia mtu anasema “hii kazi haina maslahi” na haangalii kama Mungu anataka nini ila pesa tu, ni hatari. Sio kila wakati utafanya kazi kwa malipo ya pesa, Mungu anaweza kubadili mfumo wa malipo kwa baadhi ya kazi. Usipokua makini unaweza kujikuta unajifungia milango ya muhimu wakati unakimbiza pesa na ukajikuta hufiki mbali. Pamoja na kufanya faida, REHEMA iwe ndio mhimili wa maamuzi yako ya ki-PESA au kuhudumia wateja wako.

2. Mfumo wa duniani utakulazimu kufanya mambo mabalimbali wakati wa kufanya HUDUMA na mengine ni magumu. KUMBUKA wewe ni MTUMISHI (mtumwa), kuna Bwana aliyekutuma. Ukibinafsisha HUDUMA ikawa yako itakua NZITO mabegani mwako. Kwa maana kila HUDUMA ina VITA, na Maandiko yanasema HAKUNA askari aendaye VITANI kwa GHARAMA zake! Ukifika mahali pa kujisahau ukaanza kusema “huduma yangu” huku ukisahau kua wewe ni MTUMWA na sio BWANA (boss) au MMILIKI wa hiyo HUDUMA unakaribia kufikia MAHALI pa gumu. Hata siku moja USISAHAU kwamba kuna “organization structure” ya Mungu ambayo yeye ni TOP BOSS na sisi ni vibarua tu. Sasa hapo juu yako kunaweza kua na VIONGOZI wako wa KIROHO, chunga usiwavunjie HESHIMA na ukakosa kuwasikiliza kwa KISINGIZIO cha HUDUMA na UPAKO juu yako. Imempasa KILA mmoja kuitii mamlaka iliyo kuu katika KAZI ya HUDUMA na ni vyema sana ukaitambua mamlaka “inayokuhusu” na kukaa VIZURI nayo maana inaweza ikawa SABABU ya wewe KUKUA au KUANGUKA kihuduma. Katika MFUMO huu wa Utawala, jua kuna wakati utakua na watu chini yako. ANGALIA basi kwa sababu na sisi tu wa BWANA wetu ambaye tunamtumaini KUTUBARIKI nasi tusizuie mkono wetu kuwabariki walio chini yetu na kuwatanguliza kama BWANA wetu alivyotupa mfano wa kunawisha miguu wafuasi wake. Ukitaka kua BOSS/MKUU sharti ujifunze “kuvua nguo (utukufu) na kujifunga taulo kiunoni KISHA “kuinama” (kunyenyekea) na kuwanawisha (kuwatumikia) MIGUU michafu walioko chini yako kwa USTAHIMILIVU”.

3. Katika mfumo wa kufanya kazi ya Mungu utahitaji VIBALI na michakato mingi ya KISHERIA na imekupasa kumpa KAISARI kilicho chake kwa UAMINIFU wote. Huwezi kuepuka wezi, nondo na wadudu mbalimbali (ma-promota, producer, nk.) walao maadam uko duniani. Ila jua Bwana ni fungu lako na HUTAPATA hasara kwa maana yeye anaona SIRINI na anajua shida yako na ATAKUJAZI. Kumbuka kuweka HAZINA yako Mbinguni pia maana huko hakuna kutu, nondo wala wezi. Na unahitaji ULINZI wa Mungu ili HUDUMA yako “isipukutishe majani/maua” kabla ya KUZAA, na yeye anaweza pia KUMKEMEA yeye ALAYE (Ibilisi na watu wake), ulinzi huu unaupata katika ZAKA KAMILI! Jifunze KUTOA kwa USAHIHI maana kuna faida NYINGI.
Warumi 13: “1 Hivyo amwasiye mwenye mamlaka hushindana na agizo la Mungu; nao washindanao watajipatia hukumu. 2 Kwa maana watawalao hawatishi watu kwa sababu ya matendo mema, bali kwa sababu ya matendo mabaya. Basi, wataka usimwogope mwenye mamlaka? Fanya mema, nawe utapata sifa kwake; 3 kwa kuwa yeye ni mtumishi wa Mungu kwako kwa ajili ya mema. Lakini ufanyapo mabaya, ogopa; kwa maana hauchukui upanga bure; kwa kuwa ni mtumishi wa Mungu, amlipizaye kisasi mtenda mabaya kwa ajili ya ghadhabu. 4 Kwa hiyo ni lazima kutii, si kwa sababu ya ile ghadhabu tu, ila na kwa sababu ya dhamiri. 5 Kwa sababu hiyo tena mwalipa kodi; kwa kuwa wao ni wahudumu wa Mungu, wakidumu katika kazi iyo hiyo. 6 Wapeni wote haki zao; mtu wa kodi, kodi; mtu wa ushuru, ushuru; astahiliye hofu, hofu; astahiliye heshima, heshima. 7 Msiwiwe na mtu cho chote, isipokuwa kupendana; kwa maana ampendaye mwenzake ameitimiza sheria.”

4. Huwezi kufanya HUDUMA na kutumia VIPAWA vyako bila kuwa na watu wengine katika timu. Huduma inavyozidi kukua utahitaji watu wengi zaidi. Kumbaka jambo hili siku zote, wana wa Mungu wanapojihudhurisha mbele za Mungu wao, shetani naye huja kati yao. Ni vigumu sana kutambua magugu yawapo pamoja na ngano na sio kazi yetu “kuyang’oa” maana hakuna aliyepewa huo wito na BWANA wetu ila inabidi kujichunga na kujilinda na “chachu” yao maana inaweza kuchachusha HUDUMA yako bila kujua. Yesu alikua na wanafunzi 12 na mmoja wao aliitwa “msaliti”! Kama Yesu alikuwa na timu na ndani yake kuna YUDA, jua imekupasa kuwa makini na macho ya mwili na roho kujua watu wa timu yako maana humo watakuwepo wasaliti na wengine ni hatari kuliko YUDA. Kazi ya Yuda ilikua “mweka hazina” ila alikua akiiba vitu/matoleo! Sasa chunga sana mienendo na tabia za watu wa timu yako maana jua kuna roho nyuma yao na mwisho wake huwa ni KUSALITI ili huduma ife bila kujali madhara. Kipimo kikubwa cha uaminifu wa wengi katika timu ni TAMAA ya pesa! Hii ndio ilimfanya YUDA akasaliti huduma yao na Bwana wake kwa sababu ya KIPATO cha vipade 30 tu vya fedha! Sasa jua neno hili kwamba kama YUDA ambavyo hakuila ile pesa, ndivyo wengi sana wanaomsaliti Bwana aliyewatuma huishia pasipotarajiwa kama ilivyokua kwa YUDA au zaidi. Ndani ya vikundi vingi sana wamejipenyeza akina Delilah na wamenyongelea chini HUDUMA nyingi na imebaki mazoea tu na nguvu ya ugali. Imekupasa kukaa katika Maombi ya DHATI kabisa kama timu nzima na kuwa na ratiba za KULA na kujifunza na KUSIKILIZA maagizo ya Bwana aliyewatuma kazini ili msiingie majaribuni.

5. Chanzo cha nguvu zetu ni Mungu aliyetutuma kwenye kazi yake. Huwezi kumchanganya Beliari na Mungu na ukapata matokeo mazuri. Ni jambo la kustaajabisha sana kuteremkia Misri kutafuta msaada ili usimamishe HUDUMA! Yaani unamsaidia Mungu “kutafuta msaada au mtaji kutoka kwa mungu mwingine”! Kumbuka, kukua kwa huduma ni hatua, ambazo huongozwa na Mungu. Na kukua huku kunaenda sambamba na kukua kwa IMANI yako. Kama unataka kukua kwa kasi basi kimbiza kukua kwa IMANI yako. Kwa maana “tunafanikwa katika mambo YOTE kwa kadri roho zetu zifanikiwavyo”. Kwa MAJIRA na vipindi alivyoamuru Mungu, ataleta mtaji na mahitaji ya kukuza huduma yako. Ukifika mahali “unakopa” na kujitaabisha sana ili “uwekeze” kwenye huduma kwa malengo ya KUKUA KWA HARAKA, jua unakaribia mahali sio pazuri. Kama wewe ni “mtumwa” na Bwana wako anataka ulime hatua 10 kwa siku, kwanini ushindane naye na kutaka kulima hatua 100? Je! Hizo hatua 90 za zaidi ulifanya kwa msukumo wa kumzalishia Bwana wako au “kujiongezea kipato”. Jiulize kinachokusukuma ni BIASHARA au HUDUMA? Sasa usiwe MLEGEVU katika kazi ya BWANA maana Mungu amekataa UVIVU na ULEGEVU ila tuwe na BIDII katika KUTAFUTA na KUTENDA mapenzi ya Mungu peke yake.

6. Ukiona UNAMTUMIKIA Mungu, na umefika mahali ukitaka PESA kwa ajili ya jambo fulani, na unajikuta UNACHANGISHA watu, au kuomba watu PESA “kabla” ya kumwomba “kwanza” Mungu hiyo PESA, jua unakaribia mahali pa GUMU. Epuka kua OMBAOMBA na jifunze kumtegemea Mungu kama kweli UNAMTUMIKIA Yeye. Yesu alipotaka “pesa” alituma mtu akavue samaki na kisha ampasue atoe huko sarafu! Unadhani wakati wa Yesu akina ZAKAYO hawakuwepo? Unadhani alishindwa kuwambia tu kwa URAHISI walete SADAKA/MBEGU na wakamjazia kila mahali MIJI-HELA? Angalia basi Mtumishi wa Mungu usije ukahamisha TEGEMEO lako kwa wanadamu bila kujua. Ni kweli Mungu atainua hata “mawe” yafanye kazi yake, ila chunga usije ukaanza na kutafuta misaada kwa “mawe” kama hayo ndio yamekuita katika kazi ya HUDUMA. Muombe Mungu kwa bidii, tafuta USO wake kwa bidii zote, kama atatuma MALAIKA kukuletea “mkate na gudulia la maji” au kama atatumia KUNGURU kukuletea “mkate” kama kwa Elia Mtishibi, sio juu yako kuchagua. Mtumaini yeye na kaa katika KUSUDI lake. Mojawapo ya sifa za watu wanaomtegemea Mungu katika VIPATO vyoa ni KUOGOPA sadaka na KUIHESHIMU! Yamkini hujawahi kukutana na mtumishi wa Mungu anakataa SADAKA lakini wapo wengi tu, Kumbuka habari za Elisha baada ya kumponya mtu ukoma! Ingekua leo tungeita “sadaka ya shukurani” na tungeshangilia kupokea! Sasa sisemi sadaka za shukurani ni mbaya, ila nataka uone hii KIU ghafla ya kutaka KUPOKEA kirahisi kutoka kwa WANADAMU na KUDAI kwa nguvu au kijanjajnja saa nyingine kwa kutishia watu kwa maandiko. Hatukuitwa KUKUSANYA pesa na sadaka ila kuleta ROHO za watu kwa Mungu. Pesa ikija ni sawa, ni CHAKULA CHA SAFARI tu kutuwezesha kufikilia MAKUSUDI ya Mungu na wala Pesa yenyewe sio MAKUSUDI ya MSINGI ya HUDUMA zetu labda kama tunafanya BIASHARA.

7. Majaribu lazima yaje ili kupunguza kasi ya huduma yako japo ukiyashinda UNAPANDA cheo. Kwa Ayubu shetani alisema “nikigusa kitu cha karibu naye” huyu jamaa lazima ashindwe. Ibilisi akashughulikia watoto na mali zote! Usidhani ilikua mahali pa rahisi hapo kusimama tu katika UAMINIFU na Mungu. Wakati watoto wanaangamia na mali zinaporomoka wanakuja MARAFIKI “wataabishaji” wakileta injili pori na maneno “kandamizi”. Lakini Ayubu akakaza macho kumtizama Bwana wake na akafika MAHALI pa USHINDI wake, japo ilikua ni raundi ya kwanza. Raundi ya pili Ibilisi anataka kumgusa Ayubu “karibu zaidi” ili kumchanganya na kumpotezea mwelekeo. Ibilisi anasema “mwili bwana, mwili, mtu akiguswa mwilini ataachia tu ngazi”, Mungu akatoa “go ahead”. Wakati Ayubu anapambana na MAJIPU mwili mzima, anajikuna kwa kigae maana yamkini akijikuna usaha ulikua unamwagika na kigae ndio cha kukingia, huku ananuka na kwa kawaida watu wanakaa mbali, hatamaniki, MKE wake anakuja na mpya! Akidhani anamwonea huruma, akitazama haoni tena mtu ila “maiti” na anamshauri “amkufuru Mungu” kuharakisha kufa maana anaona jamaa kilichobaki ni kifo tu na anateseka bure! Ayubu alijua bado mara hii tena atafika “MAHALI pa USHINDI” wake! Kumbuka alishinda mara dufu, na alirudishiwa kila kilichopotea maradufu!

Watumishi wengi sana wameshindwa kusimama kwasababu Ibilisi amegusa vitu vya “karibu” nao. Wengine wakati wako Busy na Mungu, huku nyuma mke/mume anakamatana na makahaba! Na ibilisi ataweka “mtu wa kuleta habari” kama ilivyokua kwa AYUBU! Ili uumie na uvunjike moyo na upunguze KASI ya huduma yako. Mara nyingine “karibu” inaweza kua watoto, wazazi, ndugu, mali au ajira alimradi ni mahali PATAKAPOKUGHARIMU na PANAUMA. Lengo ni kukukatisha tamaa mtu wa Mungu ili ukose mwelekeo na ushindwe kutimiza HUDUMA au kuzaa MATUNDA sawa na wito au KIPAWA chako. Chunga sana hili eneo maana ni gumu na limefisha HUDUMA nyingi sana za watumishi wa Mungu na wameshindwa kuzaa MATUNDA yawapasayo. Sikiliza MTUMISHI wa Mungu, KILA kitu kitapita, usiangalie kushoto wala kulia, kama ni mume au mke amekusaliti kwa kumsikiliza Ibilisi na kwa “kutokujua saa ya kujaribiwa kwake”, wewe USIKATE tamaa, SONGA mbele! Mwangalie Mungu aliyekuita na uzidi katika nguvu zake na mapenzi yake maana hapo ndipo MAHALI pa USHINDI wako.

Kwa sababu kila mtu katika Mwili wa Kristo ameitwa kwa kazi maalumu kama ilivyo viungo vya miili yetu, basi jua kama UNASHIKA njia za SHETANI sio tu kwamba UNAHARIBU huduma yako, ila pia UNAANGAMIZA huduma ya watu wa “karibu” wanaokuhusu kwa sababu kwa KUTENDA hayo MAOVU unawaumiza na kupunguza KASI ya utumishi wao. Kumbuka kuukomboa wakati maana hizi ni nyakati za uovo. Msikae tu kugombana na kubishania mambo yasiyo ya msingi na kusahau kua mna KAZI shambani mwa Bwana. Mtakapo shughulika na MAMBO ya Mungu jua HAKIKA Mungu atashughulika na mambo yenu pia na BARAKA na FURAHA vitaongezeka kwenu na kwa watu wenu wa KARIBU.

Matendo ya Mitume 20: 19 “nikimtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote, na kwa machozi, na majaribu yaliyonipata kwa hila za Wayahudi; 20 ya kuwa sikujiepusha katika kuwatangazia neno lo lote liwezalo kuwafaa bali naliwafundisha waziwazi, na nyumba kwa nyumba, 21 nikiwashuhudia Wayahudi na Wayunani wamtubie Mungu, na kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo. 22 Basi sasa, angalieni, nashika njia kwenda Yerusalemu hali nimefungwa rohoni, nisiyajue mambo yatakayonikuta huko;
23 isipokuwa Roho Mtakatifu mji kwa mji hunishuhudia akisema, ya kwamba vifungo na dhiki vyaningoja. 24 Lakini siyahesabu maisha yangu kuwa kitu cha thamani kwangu kama kuumaliza mwendo wangu na huduma ile niliyopokea kwa Bwana Yesu, kuishuhudia Habari Njema ya neema ya Mungu. 25 Na sasa, tazameni, mimi najua ya kuwa ninyi nyote niliowahubiria ufalme wa Mungu, nikienda huko na huko, hamtaniona uso tena. 26 Kwa hiyo nawashuhudia wote siku hii ya leo, ya kuwa mimi sina hatia kwa damu ya mtu awaye yote. 27 Kwa maana sikujiepusha na kuwahubiria habari ya kusudi lote la Mungu. 28 Jitunzeni nafsi zenu, na lile kundi lote nalo, ambalo Roho Mtakatifu amewaweka ninyi kuwa waangalizi ndani yake, mpate kulilisha kanisa lake Mungu, alilolinunua kwa damu yake mwenyewe.”

8. USHUHUDA. Kama kuna kitu kimekwamisha kazi ya Mungu ni USHUHUDA mmbaya wa watumi wa Mungu. Kumbuka, unapotenda “KITUKO” chochote hadharani au kwa SIRI ila Ibilisi amefanikiwa kukichomoza hadharani, watu wataanza kukutizama kama wewe ni mtu wa “namna ile” sawa na KITUKO ulichofanya, hata kama ilikua mara moja. Ile LEBO unayobandikwa ya hiki KITUKO ina tabia ya KUDUMU na ni NGUMU sana kuifuta kwa jinsi ya kibinadamu. Sababu ya msingi hapa ni kwamba Mungu ANASAMEHE na hakumbuki kama UKITUBU, ila wanadamu HAWASAHU hata kama umetubu. Kama ulifanya UZINZI bado watu watakutizama tu kama MZINZI kwa muda mrefu. Ibilisi naye atahakikisha habari MABAYA inaenea kwa KASI kwa sababu yeye ni “mshitaki”. Watu wengi sana wamesahau kwamba USHUHUDA ni silaha ya MUHIMU kumshinda Ibilisi, ndio maana tunasoma “nao wakamshinda kwa Damu ya Mwana-kondoo na kwa neno la ushuhuda wao..” Kama kuna kitu Ibilisi anawinda ni kupata USHUHUDA wako mmbaya na KUUSAMBAZA kila mahali. Unaposimama KUHUDUMU anawakumbusha watu na kuwaambia “msimsikilize huyu jamaa kwanza ni tapeli/mzinzi/mrushi/mwizi” nk. Mara nyingi sana watu wameshindwa kupokea Neema ya Mungu iokoayo na hata kusema kwa ujasiri “hakuna wokovu duniani” kwa sababu wanajua WALICHOONA kwa wana wa Mungu. Makosa ya ZAMANI yana NGUVU ya kuzuia MAFANIKIO yako ya sasa na ya baadae KIHUDUMA kama hujawa makini na kutafuta Neema ya kupona na MAMBO ya KALE.

Kwa upande mwingine, sio kila jambo jema laweza kuwa na USHUHUDA mzuri. Kwa lugha nyingine, sio tu kwamba USHUHUDA mmbaya ni kuanguka dhambini. Kuna mambo mengi sana katika mienendo na tabia ambayo Paulo alisema katika kitabu cha Warumi kua makini nayo. Kuna mambo IMEKUPASA kuacha kufanya kwa sababu ya UDHAIFU wa imani ya mtu mwingine sio imani yako. Mfano rahisi ni namna ya UVAAJI wa nguo. Watu wengi wameonekana kama WAHUNI tu kwa sababu ya aina ya nguo walizovaa na MUONEKANO wao katika mavazi hayo. Na wengine wamekua wabishi na kiburi hata wakiambiwa au wakionywa! Mungu atusaidie tusiwe KWAZO kwa namna yoyote. KUMBUKA kumpokea dhaifu wa imani na kumsaidia sio kumwangamiza kwa UDHAIFU wa imani yake eti kwa sababu sisi ni MIAMBA ya Imani. Hicho ni KIBURI.

NEEMA ya BWANA na IZIDI KWENU TANGU SASA na HATA MILELE. AMEN.

Frank Philip

Monday, December 2, 2013

PIMA HATUA ZAKO!!!



Ukitaka kujua umbali au kimo utakachofikia kiroho angalia aliko kiongozi wako wa KIROHO. Kwa maana yatosha mwanafunzi kulingana na mkufunzi wake ila hampiti.

Sasa nisikilize vizuri. Kila ajikwezaye atadhiliwa naye ajidhiliye atakwezwa. Ninazungumzia tabia ya ndani ya unyenyekevu ambayo Mungu anaipenda. Kupitia tabia hii mtu huinuliwa na kuwa MKUU kuliko wenzake kwa kukubali kuwa MDOGO kuliko wenzake. Kuna kundi dogo la watu ndani ya Kanisa ambao wao watanyenyekea chini ya Mkono wa Mungu na viongozi wao. Kama wamezingatia mambo matatu yafuatayo kati ya mengi watafika mbali: 1. watautafuta uso wa Mungu kwa BIDII, 2. wataacha uovu na kusafisha njia zao mbaya 3. watatafuta kusudi la Mungu hata kama hawapati faida kwa jinsi ya mwilini. Sasa hili kundi dogo, kwa maana ni dogo kweli, litajikuta na nguvu nyingi sana za kiroho na watafanikiwa kwa jinsi ya rohoni na mwilini kwa kadri watakavyokaa katika kusudi la Mungu.

Mambo kadhaa yatajitokeza.
1. VITA na VIPINGAMIZI kutoka kwa viongozi wao na watu wengine kwa sababu ya wivu. Hali hii ya kuinuliwa ikiibuka katika kundi hili dogo, wapo watakaovumilia na kunyenyekea na kudumu hapo chini ya viongozi wao na wengine wataondoka na kuanzisha huduma au kujiunga na viongozi wengine. Sasa hii ni hali ya kawaida sana kwa nyakati tulizo nazo kuwa na makundi ya namna hii.TAHADHARI! kwa lile kundi linalohama kwa sababu ya MADHAIFU ya walikotoka. Angalia usihame kwa KIBURI ila uhakikishe ni makusudi ya Mungu juu ya maamuzi unayofanya maana unaweza kujikuta umepoteza ile nguvu uliyodhani unayo. Katika hili twajifunza pale ambapo Yesu alipoanza huduma, na nguvu za Mungu kudhihirika sana katika maisha yake, vita iliibuka kwa wakuu wa DINI. Kumbuka, Yesu hakufanya kitu ambacho hakumwona Baba yake anafanya, ilikua ni mapenzi ya Mungu kabisa ila VITA ilikuwa kali. Kila mtu asimamaye katika mapenzi ya Mungu kwa uelekevu na kumpendeza LAZIMA Mungu atajidhihirisha kwa maana “jicho la Mungu linakimbia-kimbia duniani kote kumsaka mtu wa namna hii ili Ajionyeshe mwenye nguvu”. Usistushwe uonapo vita wakati unajua ufanyacho ni mapenzi ya Mungu. Simama katika nafasi yako kwa unyeyekevu na fanya huduma uliyoitiwa kwa uaminifu.
2. Mungu atawapa hili kundi dogo nguvu za maamuzi katika kanisa au huduma wanakotumika. Kwa kadri hili kundi dogo linavyojinyenyekesha na kumtii Mungu, Mungu atawapa hekima na maarifa hata na nguvu za kiuchumi kiasi kwamba hawa VIONGOZI watawatafuta kwa ushauri, msaada na mambo mengine ya kihuduma na mwishowe kama hawa WAKUU wanazidi “kulala”, maamuzi mengi au makubwa yatategemea hili kundi dogo la watu walioamua kumpendeza Mungu na kuutafuta uso wake kwa bidii hata kama majina yao hayapo kwenye orodha ya mashemasi, au watu wowote wenye vyeo kanisani. Kumbuka mfano wa Paulo. Japo alikuwa mfungwa kati ya wafungwa wengine na wasimamizi wao, wakati wanasafirishwa baharini yeye alikuwa ndio anasema cha kufanya na watu wanamsikiliza kwa sababau kwa wakati huo ndiye aliyekuwa amesimama na mapenzi ya Mungu peke yake na anatenda makusudi ya Mungu hata kama ni mfungwa.


Wakati VIONGOZI wengi sana wanasahu kazi ya “mchungaji wa kondoo” na wanageuza hiyo huduma kama “mchungaji wa mshahara”, hawatajua ni saa ngapi hili kundi dogo limekamata usukani na kusukuma kazi ya Mungu mbele wao wakiwa busy na miradi yao. Jipange katika nafasi yako na ni MARUFUKU kumnyooshea mtumishi wa Mungu kidole. Fanya kazi ya huduma na ONGOZWA na Mungu. Kama jinsi DAUDI alivyosimama katika nafasi yake wala hakushindana na Mfalme SAULI japo alitaka kumwangamiza, kaza macho yako katika WITO wako na acha VITA na wanadamu. ADUI yetu ni Ibilisi peke yake! Daudi hakufurahia kuanguka kwa Sauli japo kibinadamu Sauli alikuwa ADUI kwa Daudi! Alijua japo yeye amepakwa MAFUTA ila alihehimu nafasi ya SAULI hadi wakati wa Bwana ulipotimia. Na aliomboleza KIFO cha SAULI, hakufanya SHEREHE kwa sababu alijua kwamba pamoja na madhaifu ya SAULI, bado alikuwa ni MASIHI wa BWANA! Uwe makini Mungu anapokuruhusu kuona MADHAIFU ya watumishi wa Mungu!

Mara nyingi sana watu wamejisahau na kufikiri MUSA atadumu milele! Yamkini wewe ni Joshua au Kaleb na hujitambui. Na mara nyingine kuna watumishi kama Eliya ambao wanadhani wengine wote wamekwisha na wako wenyewe kwenye HUDUMA, kumbe Bwana amejisazia Elfu saba wasiopiga goti kwa Baali. Hapa nazungumza na hawa Elfu saba, Joshua na Kaleb. Wamo katika kundi kubwa la WALIOITWA na watafuata kuchukua MIKOBA ya VIONGOZI wao na kupeleka kazi ya Mungu mbele. Mara nyingi hawa watu hawaandaliwi na mtu, Mungu huwaandaa mwenyewe na atakupaka mafuta huko huko MACHUNGANI kama Daudi. Wakati unapambana na DUBU na SIMBA, jua unaandaliwa KUMSHUGHULIKIA Goliath katika KIZAZI chako. Baadhi watakulia miguuni pa Makuhani kama Eli kama ilivyokuwa kwa Nabii Samweli. Vyovyote itakavyokua, kama Mungu anakuaanda huko VICHAKANI kama Daudi au HEKALUNI kama Samweli, kaa katika kusudi la Mungu na jipange sawaswa maana kwa jinsi ya MWILINI wengi hawakuoni na yamkini wanakudharau kwa sabau wewe ni kijana wa kuchunga mbuzi tu ila siku UPAKO wa DAUDI unadhihirika juu yako ndipo watakapojua kuwa UKIMYA wako ulikuwa MBELE za Bwana ukijifunza na kukuwa kwa NDANI.

Neema na Rehema zitokazo juu ziwe nanyi tangu sasa na hata Milele. AMEN.

Frank Philip.

Sunday, December 1, 2013

HILA za ADUI!!!


Ukienda mnadani na ukaona NG'OMBE aliyenona na wengine wanaonekana afya mbovu. Jua yule aliyenona zaidi yuko KARIBU na KUCHINJWA kuliko huyu mwingine ambaye havutii.

Sasa unapoanza hatua za kutaka kumpendeza Mungu (KUNONA KIROHO), utashangaa ghafla watu wanakuita HANDSOME/BEAUTIFUL na wanaanza kukufanyia mambo ambayo yanakuvuta KUTENDA dhambi. Jua ADUI anataka KUKUCHINJA! Jitambe na UPONE.

Sasa, unavyozidi kua karibu sana na MUNGU unakua KIVUTIO cha ADUI na unakua mawindo. ILA kama wewe tayari ni MALI ya adui, hana haja sana KUWINDA kilicho chake! Hao watu wanaokutaka ufanye dhmbi HAWAKUPENDI ila hawakutakii MEMA! Mtu anayetaka UFANYE DHAMBI anakuangamiza na sio KUKUPENDA.

Jifunze KUJIFUNIKA kwa DAMU ya YESU na kujificha NDANI ya Yesu ili ADUI akija asikuone wewe ila Yesu. Utakua salama.

Frank Philip.